4x4

WAJUA KWA NINI HAYATI MZEE KAWAWA ALIITWA SIMBA WA VITA WAKATI WA UHAI WAKE?

Na Hamis Shimye, UPL
HAYATI Mzee Rashid Mfaume Kawawa alikuwa ni kiongozi shupavu aliyewahi kutokea, ambapo alikuwa kiongozi adhimu sana na mwenye moyo wa ajabu katika kuipigania nchi yake katika ufanyaji wa kazi mbalimbali za maendeleo.

Alikuwa ni mtu asiyeogopa kazi hadharau kazi, hana makuu, hana makundi, hana majungu. Mdogo wake akifanywa mkubwa wake atafanya kazi chini yake kwa moyo wake wote, na uwezo wake wote; bila manung’uniko, na bila kinyongo.
Katika TANU alikuwa akiitwa SMBA WA VITA. 

Haogopi maamuzi mazito. Mkishafanya maamuzi ndani ya vikao yeye basi lazima atakuwa mstari wa mbele, ambapo wengine baadaye wanaweza kusita kuyatekeleza, au wanaweza kuyatekeleza kwa shingo upande na hasa kama walikuwa hawayapendi.

Hayati Mzee Rashid Kawawa alikuwa ni mtu wa kutekeleza mambo hasa pale viongozi wakishaamua kwa pamoja, atayatekeleza kwa moyo wake wote na uwezo wake wote. Kwa ajili hiyo mara nyingi amebeba lawama peke yake kwa maamuzi ambayo yamefanywa na uongozi mzima wa Chama na serikali kwa pamoja, au ambayo nimeyafanya mimi.

Hayati Mwalimu Julius Nyerere alitoa hotuba katika mkutano maalumu wa Taifa wa CCM mwaka 1990, ambapo sehemu ya hotuba ilikuwa inamzungumzia Mzee Kawawa, ambapo Mwalimu Nyerere alisema mambo mengi ya kumsifu Kawawa.

"Nilipokwisha kutangaza kwamba baada ya kikao hiki nitang’atuka uenyekiti wa Chama chetu, Ndugu Kawawa alinijia na kusema kuwa yeye pia angependa kung’atuka. Lakini tulikubaliana kwamba si vizuri wote wawili tukang’atuka wakati ule ule. Tutakuwa kama tunamtelekeza mwenzetu. Ni bora yeye abaki ili aendelee kumsaidia mwenyekiti mpya wa Chama chetu.

Ndugu Kawawa ni Askari. Hajitafutii madaraka; lakini hasiti kupokea madaraka yoyote anayopewa na chama chake.

Ndugu Kawawa, sijui jinsi ya kukushukuru kwa niaba yangu mwenyewe na niaba ya nchi yetu na Chama. Kwangu mimi imekuwa ni bahati na faraja ya pekee kwamba kwa muda wote wa uongozi wangu umekuwa makamu na msaidizi wangu. Unastahili kupumuzika, kama mwenyewe ulivyoomba. 

Badala yake tunakuomba uendelee kumsaidia mwenyekiti na Rais wetu; na hivyo uendelee kukisaidia Chama chetu na Nchi yetu. Umekubali Ahsante sana".

*Hotuba aliitoa Mwalimu Nyerere katika mkutano Mkuu Maalum wa Taifa, Agosti, 1990.

0 comments:

Post a Comment