4x4

RAIS DK. MAGUFULI AMTUMBUA MKURUGENZI MTENDAJI TANESCO LEO

Na Bashur Nkoromo, Dar
Rais Dk. John Magufuli, leo amemtumbua Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mhandisi Felchesmi Mramba, katika hali inayoonesha kuwa Rais amekerwa na jaribio la Tanesco kupandisha bei ya umeme kuanzia leo, Januari Mosi, 2017.

Taarifa iliyotolewa leo na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu jijini Dar es Salaam, imesema, kufuatia kutenguliwa kwa uteuzi huo, Rais Magufuli amefanya 'bandika pandua' kwa kumteua Dk. Tito Esau Mwinuka kuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO.

"Kabla ya uteuzi huo Dk. Tito Esau Mwinuka alikuwa Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM)
Uteuzi wa Dkt. Tito Essau Mwinuka unaanza mara moja", imesema taarifa hiyo ya Ikulu iliyosainiwa ana Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Gerson Msigwa.

Hatua ya Rais Magufuli, imekuja ikiwa ni siku mbili baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuiidhinisha ongezeko la asilimia 8.5 ya ya bei ya huduma za umeme kwa kilichoelezwa kuwa lengo ni kukidhi gharama za uzalishaji wa umeme.

Ongezeko hilo lilitangazwa juzi jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngamlagosi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maombi ya kurekebisha bei za umeme ambayo yalitarajiwa kuanza kutekelezwa leo, Januari Mosi, 2017.

Ngamlagosi alisema, kuwa TANESCO iliomba kuidhinishiwa ongezeko la bei ya huduma hizo ili kuliwezesha shirika hilo kupata fedha za kulipia gharama za uendeshaji, kupata fedha za uwekezaji katika miundombinu pamoja na kuhakikisha huduma ya umeme inawafikia asilimia 75 ya wananchi wote ifikapo mwaka 2025.

”Baada ya TANESCO kuwasilisha taarifa zinazohitajika kwa ajili ya kukamilisha maombi yao, EWURA ilifanya mikutano ya taftishi, matangazo kwa umma pamoja na kushirikisha wadau mbalimbali kutoa maoni juu ya ongezeko hilo ambapo baada ya uchambuzi wa maoni hayo tulilidhia kuongeza asilimia 8.5 tu ya ongezeko la bei hizo ,” alisema Ngamlagosi.

Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) ambalo linanunua umeme wa jumla kupeleka Zanzibar limeongezewa asilimia 5.7 ya bei ya umeme badala ya asilimia 19.1 iliyoombwa na TANESCO.

Alisema kulingana na marekebisho yaliyofanyika, jumla ya mapato yanayohitajika kwa mwaka 2017 ni sh. bilioni 1,608.47 ambayo yamesababisha ongezeko la bei la wastani wa asilimia 8.5 hivyo gharama za umeme zimeongezeka kutoka sh. 242.34 kwa uniti moja hadi sh.  263.02 kwa uniti moja.

Mkurugenzi huyo alitoa maagizo kwa TANESCO yakiwemo ya kuanzisha tozo ya mwezi ya sh. 5,520 kwa wateja wa kundi linalohusisha viwanda vidogo, mabango na minara ya mawasiliano, kuboresha huduma kwa wateja pamoja na kuacha kuwaunganisha wateja wadogo kwenye kundi la wateja wakubwa na badala yake kuwaunganisha moja kwa moja katika kundi la wateja wadogo.

Aliwataka wananchi kuelewa kuwa kundi linalojumuisha wateja wa majumbani ambao matumizi yao ya umeme hayazidi uniti 75 kwa mwezi hawataathirika na ongezeko hilo la bei.

Uchunguzi uliofanywa na Mtadao huu, umebaini kuwa zipo familia nyingi zenye uwezo mdogo ambazo kwa mwezi matumizi yake ya umeme hufikia hadi uniti 150 kwa mwezi, na pia tofauti na inavyoeleza kuwa wananchi wa kawaida wasigeathirika na kupanda kwa bei hiyo ya umeme, maoni ya wadau yameonyesha kuwa watu hao wangeathirika kutokana na bei za bidhaa ambazo zingepanda bei kufidia gharama ya umeme. 

0 comments:

Post a Comment