4x4

MAKALA: CHAMA CHA DEMOKRASIA NA UBAKWAJI WA DEMOKRASIA HALISIA

Mathias Canal (Picha na David Mtengile
CHAMA CHA DEMOKRASIA NA UBAKWAJI NA DEMOKRASIA HALISIA

Na Mathias Canal
Katika sehemu ya maelezo yake Raisi wa 16 wa Marekani Bw Abraham Lincoln namnukuu aliwahi kusema kuwa Demokrasia ni mfumo wa serikali ambapo wananchi wote ni sawa mbele ya sheria na wanashiriki katika kufanya maamuzi ya kitaifa juu ya masuala ya umma. Wakati mwingine wananchi hushiriki moja kwa moja - hii ina maana kwamba wao hupiga kura moja kwa moja kwenye masuala kama vile katika chaguzi. 

Kabla sijaanza kuzungumzia uchaguzi wa CHADEMA Kanda ya Nyasa Tutazame Mwongozo wa kumteua muaniaji Urais nchini Marekani Kabla ya Wamarekani kuamua nani wanayemtaka awe rais ajaye, wao kwanza huteua nani atakayewania kiti hicho.


Mchakato huo hungo'oa nanga kwa mchujo wa kamati za wajumbe ambapo wananchi hupata fursa ya kumchagua muaniaji kiti cha urais kwa tiketi ya chama cha Democratic au kile cha Republican.Mshindi wa mchujo huo huwakusanya wajumbe - hawa ni wanachama wenye nguvu ya kupiga kura kumchagua mgombea katika mikutano ya chama.

Nchini Marekani inakumbukwa kuwa kulikuwa na upinzania mkali katika uchaguzi wa nafasi ya Rais kati ya vyama viwili ambapo ni Republican na Demokratic, Kwa upande wa Democrats upinzani mkali ulikuwa kati ya Hillary Clinton na Seneta Bernie Sanders ambaye alionekana nae kupata uungwaji mkono zaidi dhidi ya Clinton. Kwa upande wa Republican kulikuwa na wagombea kama Marco Rubio na Ted Cruz sambamba na Donard Trump aliyeibuka kuwa mshindi wa chama hicho na mshindi wa nafasi ya Urais wa Marekani.

Tutakubaliana wote kwa pamoja kwamba Vyama vyote nchini Marekani vilisimamisha wagombea katika kura za awali kabisa ambao wote kwa pamoja walipigiwa kura na wajumbe wao hapakuwa na kura za Ndio na Hapana kwa maana ya Kivuli/Jiwe na Mtu sasa tutazame mchakato ulivyo kuwa kwenye vyama vinavyounda umoja wa katiba ya Wananchi UKAWA vikiongozwa na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA jinsi vilivyompata mgombea wake wa Urais.

Julai 30, 2015 nikiwa natazama Luninga majira ya saa tatu na dakika moja usiku niliona katika kipindi cha Dira ya Dunia kinachorushwa na chombo cha habari cha BBC kupitia Televisheni ya Star Tv kikiarifu kuwa WANACHAMA wapya wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa pamoja na na Juma Duni Haji wamepitishwa katika Mkutano Mkuu wa chama hicho kugombea ngazi ya urais na umakamu wa rais kwa asilimia 99.3 ambapo jumla ya wajumbe 2021 kati ya 2035 waliotakiwa kuhudhuria kwenye mkutano huo, walipiga kura za NDIO kwa kuwa hapakuwa na wagombea wemngine na kuibua kishindo katika mkutano huo uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.

Awali kabla ya kufanyika uchaguzi huu Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa Mhe Freeman Alikael Mbowe Akizungumzia utaratibu wa kuteua mgombea huyo alisema kuwa, kwa mujibu wa katiba hiyo kifungu namba 7.16, mgombea urais pamoja na makamu wake wanateuliwa na sio kupigiwa kura.

Yaani kama kuna mtu hakuelewa vyema hapo katika maelezo hayo naomba nimsaidie kwa hili naamini ataelewa vyema zaidi Mbowe alisema kuwa kwa mujibu wa katika huku akitaja kifungu Mgombea Urais hapigiwi kura na wajumbe bali anateuliwa. Hii ni kauli ya kishujaa nay a ubakaji wa Demokrasia kwa uwazi kabisa.

Tujikumbushe Demokrasia ni nini kabla ya kuendelea na mjadala ili tuende sawa: Utawala wowote wa Demokrasia ni ule unaotokana na ridhaa ya wananchi, ambao kutokana na utaratibu waliojiwekea hufanya maamuzi ya kuwapata viongozi wao. Wananchi hushiriki moja kwa moja - hii ina maana kwamba wao hupiga kura moja kwa moja kwenye chaguzi. Tukubaliane sasa ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA hakuna Demokrasi kama ambavyo inahubiriwa katika vijiwe na majukwaa ya kisiasa. Na kama demokrasia ni pamoja na kushirikisha wananchi kufanya maamuzi kwa nini Mbowe aliamua yeye kwamba Lowassa na Duni wateuliwe sio kupigiwa kura na wajumbe zaidi ya 2000, kwa akili ya kawaida tu na karne hii unaweza kuwaambia watu fanyeni maamuzi kati ya Jiwe/kivuli na mtu...? Lakini katika hili sikuwaona vijana wa CHADEMA wakihoji wala wale wa Umoja wa Kizazi cha Kuhoji (UTG) wakihoji. Huenda walipitiwa hawakuliona hili sasa tuendelee.

UCHAGUZI KANDA YA NYASA 

Kwa kunukuu gazeti la Rai linalochapishwa na KAMPUNI ya New Habari (2006) Ltd ambayo pia inachapisha magazeti ya Mtanzania, Bingwa, Dimba na The African, la Disemba 8, 2016 liliandika habari ilikuwa na kichwa cha habari kilichosema UCHAGUZI CHADEMA NI ‘VITA’ KALI 

‘NI vita’, hivyo ndivyo tafsiri inapatikana kufuatia mvutano mkali ulioibuka ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kati ya Mchungaji Peter Msigwa na Patrick Ole Sosopi ambao walikuwa wanapambana kuwania nafasi ya uenyekiti kanda ya Nyasa.

Msigwa ambaye ni Mbunge wa Iringa Mjini alipamba na kijana Machachari katika Siasa za Tanzania Patrick Ole Sosopi ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), kuwania Kanda hiyo ya Nyanda za Juu Kusini (Nyasa) inayojumuisha mikoa ya Iringa, Mbeya, Rukwa, Njombe na Songwe.

Tangu maandalizi ya uchaguzi kanda nane za Chadema yalipoanza mwezi uliopita kulikuwapo na majibizano kati ya wafuasi wa wagombea hao wawili ambao kwa namna moja au nyingine wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii kuanika madhaifu ya kila mgombea.

Hata hivyo, Msigwa alionekana kushambuliwa zaidi na wafuasi wa Chadema Kanda ya Nyasa kutokana na madai mbalimbali ikiwamo tabia ya kutoshirikiana na wabunge wenzake katika kukijenga chama, pia kujiweka mbali na wabunge wa chama hicho kipindi walipokuwa wakipambana kutetea madai yao kwa Naibu Spika wa Bunge Dk. Tulia Ackson.

Kwa mujibu wa taarifa zilizolifikia gazeti la RAI zinaeleza kuwa baadhi ya wabunge na viongozi wa chama hicho walionekana kusita kumuunga mkono Mbunge huyo kutokana na madai ya ubinafsi aliouonyesha katika kipindi cha kampeni za uchaguzi mkuu 2015 kwa kushindwa kushirikiana na makada wa chama hicho kuzunguka sehemu mbalimbali.

Hata hivyo baadhi ya wafuasi wa Ole Sosopi walionekana kulalamika kutukanwa kwenye mitandao ya kijamii ambapo mmoja wao alisema: “Nimeshangaa sana watu kunifuata inbox na kunitukana hata wengine kutumia lugha ambayo si njema. Kumuunga mkono Sosopi ‘it’s just my perception.’ Kwa kuwa nina akili timamu siwezi kujibu matusi kama mlivyofanya “Imeniuma sana, nimeumia sana. Naomba niliweke wazi hili, Peter Msigwa ni Mbunge wangu, ni mlezi wangu na sina ugomvi naye. Sosopi na Msigwa wote ni Chadema na wote ni familia moja ndani ya chama chetu Chadema,” 

SIKU YA UCHAGUZI WA KANDA YA NYASA

Tarehe Disemba 22, 2016 ndio siku ambayo Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA kilifanya uchaguzi huo lakini mapema asubuhi kabla ya kuanza kwa uchaguzi jina la Patrick Ole Sosopi liliondolewa katika kinyang’anyiro cha kugombeanafasi ya uenyekiti Kanda ya Nyasa na Uongozi wa Kamati kuu ya Chama hicho iliyokuwa inaongozwa na Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa Freeman Alkael Mbowe.

Sosopi alipewa taarifa kwa njia yam domo kwamba jina lake limetolewa pasina kupewa hata maelezo kwa njia ya maandishi lakini pia taarifa hiyo alipewa asubuhi siku ya uchaguzi sio siku moja ama mbili kabla ya uchaguzi
Aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Ubungo ambaye kwa sasa ni katibu wa Nec, Itikadi na Uenezi wa  CCM Taifa Hamphrey Polepole aliwahi kusema kuwa Huu si wakati wa siasa za kutafuta uongozi; Ni wakati wa siasa za maendeleo na kujenga nchi hapo alikubaliana na dhana ya mfumo wa kupunguza madaraka kwa viongozi inayohubiriwa naserikali ya wamu ya tano chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli ya kuwataka viongozi kuwa na cheo kimoja serikalini ikibidi kuwa na cheo kimoja pia kwenye chama cha siasa isiwe zaidi ya hapo.

Kabla ya kuendelea naomba nikurejeshe katika kauli ya Mchungaji Peter Msigwa ya Mwaka 2015 aliyoisema kwamba “Raisi apunguziwe madaraka, na wakuu wa mikoa pia wana vyeo vingi sana wapunguziwe" by peter msigwa 2015.

Lakini tutazame sasa vyeo alivyonavyo mchungaji Msigwa kwenye chama na seriakli kabla ya kutazama uchaguzi wa Mwenyekiti Kanda ya Nyasa ulivyoendeshwa

Mchungaji Msigwa ni Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini

Mchungaji Msigwa ni Mjumbe wa Mkutano Mkuu Chadema
Mchungaji Msigwa ni Mjumbe wa Baraza kuu Chadema 
Mchungaji Msigwa ni Mjumbe wa Kamati Kuu Chadema
Mchungaji Msigwa ni Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Iringa
Mchungaji Msigwa ni Mwenyekiti wa Kanda ya Nyasa

Mchungaji Peter  Simion Msigwa amekipata cheo cha sita ndani ya Chadema na kuwa Mwenyekiti wa Kanda ya Nyasa baada ya wagombea wengine kuenguliwa, hivyo kuwa mgombea Pekee ambaye ni yeye Msigwa na Mgombea mwingine ambaye ni Jiwe/kivuli. Binafsi najiuliza sana lakini najiuliza kimya kimya hivi vikao vya vyeo hivyo vyote vya watu sita anahudhuriaje!


Maana ya upatikanaji wa Mchungaji Msigwa kama Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Nyasa ni kwa njia ya kuteuliwa na sio kuchaguliwa lakini Demokrasia ambayo CHADEMA huihubiri ni wazi wamekuwa wakiivunja wao maana wanawanyima nafasi wagombea pendwa na kukata majina yao na hatimaye wanakubali mgombea mmoja ashindane na kivuli pamoja na kwamba hakubaliki.

UCHAGUZI WA CHADEMA KANDA YA NYASA ULIKUWAJE BAADA YA MSIGWA KUBAKI MGOMBEA PEKEE AKISHINDANA NA KIVULI CHAKE MWENYEWE

Kwa mujibu wa andiko la lililosomeka kama “NIMEAMINI MAISHA BILA UNAFIKI HAYAENDI”
lililoandikwa na Mwalimu Pasaka Rucho mara baada ya mchakato mzima wa kumalizika na mshindi kutangazwa. Umeeleza tangu mchakato kuanza wajumbe walitaharuki sana kusikia taarifa ya kutolewa kwa jina la sosopi, tazama mchakato ulivyokuwa:

Wajumbe halali ni 98

Waliosusia 28
Waliopiga kura ni 106
Kura za ndio kwa msigwa 62
Kura za hapana ambazo zilipigia kivuli cha mgombea ni 44


Hii ikiwa na maana Ukichukua Kura 44 za Hapana dhidi ya Msigwa + na kura 28 za wajumbe waliosusia uchaguzi jumla yake ni =72 hivyo Sosospi tayari kama alikuwa mshindani alikuwa amejihakikishia ushindi kwa kura 78.

Kura zilizoongezeka kwa zile zilizopigwa ni 8 maana wapiga kura waliongezeka kutoka wapiga kura halali 98 na kuwa na wapiga kura wasio halali 8 waliofanya idadi kuongezeka na kuwa na wapiga kura 106.

Wajumbe waliopaswa kubaki ndani ukiondo waliokuwa wamekataa kuingia ndani ni 70

98-28=70.


Kwa maana halisi ni kwamba kulikuwa na wapiga kura 36 walioletwa na kuwa wajumbe wasio halali maana baada ya kura 44 za Hapana na wajumbe 28 kutoka ukumbini hivyo kulipaswa kupatikana kura za halali 28 ambazo ndizo kura za Ndio kwa Msigwa. 

Hii inamaanisha kwamba katika hali ya kawaida hata kama wajumbe wale 28 wasingeingia kama walivyofanya Msigwa angeshinda kwa kura 26 tu kwa maana ya wajumbe waliopaswa kubaki ndani 70- wajumbe 44 waliomkutaa=26 ambayo ndio idadi ya kura za Msigwa katika uchaguzi huo.


kwa ufupi kwa kutumia wajumbe halali katika uchaguzi kama Sosospi asingetolewa uchaguzi ungemalizika hivi:

Sosopi 72 (73.5%)
Msigwa 26 (26.5%)


HITIMISHO

Nianze kwa kumnukuu Dkt  Benson Bana wa Chuo Kikuu cha Dare s salaam ambaye amebobea katika masuala ya siasa alipokuwa akizungumza katika mkutano wa wadau wa siasa wa uimarishaji demokrasia ya vyama vingi. Alisema pamoja na mafanikio hayo bado kuna mapungufu mengi hasa ya kutokuwa na utamaduni wa vyama vingi, utamaduni unaoambatana na vyama kuwa na  aidolojia (itikadi), kukosekana kwa lugha za kistaarabu katika majukwaa ya siasa na hata mitafaruku ya ndani ya kivyama.

Mfumo wa vyama vingi ni hali ya kuwa na chama zaidi ya kimoja,katika nchi moja.Madhumuni ya kuwa na vyama vingi vya siasa ni kuleta ushindani wa kisiasa,ili kuleta maendeleo ya nchi,upinzani wa kisiasa sio uadui kama watu wengi kwenye nchi zinazoendelea wanavyodhani,kuwa na vyama vingi ni kuongeza wigo wa demokrasia katika jamii huska. Hata hivyo mara kadha amesema kuwa ili nchi yetu iweze kupiga hatua ni dhahiri lazima kuwe na Upinzani imara unaochukia Rushwa, na Uminyaji wa Demokrasia.

Binafsi sasa nakitoa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA katika Ukuzaji wa Demokrasi kwa kauli ya Mbowe kwa kusema kuwa Mgombea Urais hachaguliwi bali anateuliwa jambo ambalo ameliongoza pia kwa kumteua Mwenyekiti wa Kanda ya Nyasa Mchungaji Msigwa badala ya kuruhusu wajumbe kugombea na kuchagua kiongozi wanaomtaka.

TANZANIA ina vyama vya siasa 21 vyenye usajili wa kudumu huku kikiwepo kimoja ambacho kina usajili wa muda. Vyama hivi vimepatikana baada ya mabadiliko madogo ya Katiba yaliyotoa fursa ya kurejesha mfumo wa vyama vingi katika nchi yetu mwaka 1992.

Kufuatia mabadiliko haya, Chama cha Mapinduzi (CCM) ndicho kilichokuwa cha kwanza kupata usajili wa kudumu mwaka 1992, huku kikifuatiwa na vyama vipya vya CUF, CHADEMA,UMD, NCCR, NLD, UPDP, NRA, TADEA NA TLP vilivyopata usajili wa kudumu mwaka 1993.

Vyama vingine na usajili wao kwenye mabano ni:  UDP (1994), Demokrasia Makini (2001), CHAUSTA (2001), DP (2002), APPT(2003), Jahazi Asilia (2004), SAU (2005), AFP (2009), CCK (2012), ADC (2012), CHAUMMA (2013) na ACT (2014). RNP ni chama pekee kilichopo katika orodha ya vyama visivyo na usajili wa kudumu.

Katika vyama vyote hivi 21 mpaka sasa ni CHADEMA pekee ndicho kisichokuwa na Demokrasi kama ambavyo nimebainisha katika maeneo kadha wa kadha katika andiko langu.

Mwandishi Henry Mwangonde Aprili 23, 2014 katika gazeti la The Citizen, alimnukuu Dk. Benson Banna Katika makala yake ya “Vyama vingi vimeisaidia Tanzania” na kuandika; “vyama vya siasa nchini Tanzania havina nguvu katika kutanua mianya ya demokrasia kutokana na kukosa sera nzuri, mikakati pamoja na tabia ya viongozi wa vyama hivi kutokutumia mtaji wa wanachama wao kuviendeleza badala yake kuwatumia kwa masilahi binafsi.” Kwa mujibu wa Dkt Bana katika makala hiyo; vyama hivi vimeshindwa kutanua miaya ya demokrasia kwa kuwa havina demokrasia ndani yake.

Ni aibu kubwa sana kwa CHADEMA chama kinachojificha katika Mwamvuli wa Demokrasia katika Karne hii ya 21 kusimamisha mgombea Kivuli/Jiwe na Mtu…! Na bado kivuli kinapata kura 44? Watu 28 wanaishia mitini? Mtu anapata kura 66 naye anarudi kumsimulia Mkewe na Watoto kwamba ameshinda uchaguzi. 

Sasa hapa wachambuzi na wajuzi wa Siasa watahoji Tofauti ya CHADEMA na Yule mtu waliompa umaarufu kwa kumuita Bwana Yule upo wapi…? Lakini nimkumbushe Msigwa na CHADEMA kuwa raha na uzuri wa kura za Ndio na Hapana ni pale amabapo mshindi anaibuka kidedea kwa kura nyingi sio unapata kura 62 wakati zinakukataa ni kura 44 huku kura zingine 28 zikisusia namna ya Demokrasia ndani ya Chama.

Wakati vyama Vingine nchini vikiwa vinasonga mbele katika kuimarisha chaguzi zao za ndani ya Chama lakini CHADEMA wao wanarudi nyuma na kutoa mwanya kwa vyama vyenzake kusonga mbele.Naitazama CHADEMA kuanguka Kama umaarufu wa NCCR Mageuzi mwaka 1995.
Nitafurahi sana kuona na kusikia kauli za vijana mbalimbali wa CHADEMA wakiwemo UTG wakihoji kuhusiana na Uminyaji wa Demokrasia ndani ya chao chao CHADEMA ili tuzijue rangi zao katika kuhoji na kujenga hoja.

Mwandishi wa Makala haya ni Mathias Canal, Mchambuzi wa maswala ya jamii na siasa nchini Tanzania, Anapatikana kwa Barua Pepe ya canalmathias@gmail.com na kwa simu namba 0756413465

0 comments:

Post a Comment