4x4

HOTUBA YA MWISHO YA UZALENDO YA HAYATI MZEE KAWAWA AKISHEREHEKEA MIAKA 78

NA HAMISI SHIMYE-UPL
“Historia ya Maisha yangu ni ndefu kama ilivyokwisha elezwa. Nilizaliwa Kijijini, nikasoma Kijijini na mjini na nikafanya kazi vijijini na mjini. Katika Maisha yangu yote nimetekeleza kwa nadharia na vitendo falsafa ya UMOJA Ni NGUVU. Vitendo vimejidhihirisha zaidi katika vyama vya wafanyakazi, vyama vya ushirika na katika vyama vya siasa, hususan Tanganyika African National Union (TANU) na Baadaye Chama cha Mapinduzi (CCM). Katika Utendaji kazi, nilizingatia falsafa hii ya UMOJA NI NGUVU”.

Nikiwa na umri wa mika 23 na mtumishi Serikalini, nilijiunga na Chama cha Watumishi Waafrika Serikalini (Tanganyika African Government Servats’ Association-TAGSA). Nilijiunga na chama hicho cha wafanyakazi kwa imani kwamba UMOJA NI NGUVU. Sikuona njia nyingine ya kupambana na dhuluma za Mkoloni kwa wafanayakazi Waafrika ila kuungana na kuanzisha vyama vya wafanyakazi.

Niliamini kwamba wafanyakazi Waafrika kwa kujiunga pamoja chini ya vyama vya wafanyakazi wangeweza kupigania maslahi na haki zao kwa nguvu kubwazaidi.

Kwa kuzingatia falsafa ya UMOJA NI NGUVU, vyama vya wafanyakazi viliunda Shirikisho la vyama vya Wafanyakazi (Tanganyika Federation of Labour- TFL), tarehe 10 Oktoba,1955. 

Mimi nilichaguliwa na wenzangu kuwa katibu Mkuu wa TFL wakati huo nikitokea Chama cha Watumishi Waafrika serikalini (TAGSA).
Nilichaguliwa kwa sababu ya ujasiri na ushupavu wangu katika kupigania haki na maslahi ya Wafanyakazi kupitia Chama cha Watumishi Waafrika Serikalini (TAGSA).

Kazi ya kwanza ya TFL ilikuwa ni kuviunganisha vyama vidogo vya wafanyakazi na kuviimarisha kwa madhumini ya kuwa na nguvu na sauti kubwa zaidi. TFL haikuwa Muuongano wa Vyma vya Wafanyakazi bali Shirikisho. Vyama hivyo chini ya shirikisho viliendelea kuendesha shughuli zake vyenyewe kama vyama vilivyokuwa na madaraka kamili juu ya wanachama wake.

Kazi ya kuviunganisha na kuvisimamia vyama vya wafanyakazi chini ya TFL haikuwa ndogo hata kidogo. Nililazimika kuacha kazi Serikalini tarehe 6 Machi, 1956 ili kutumia uwezo na muda wangu wote katika kutekeleza hiyo.

Katika Kupigania Maslahi ya wanachama wake, TFL ilitumia migomo kama silaha kubwa. Migomo mingi lifanyika lakini napenda kuzungumzia kidogo mgomo wa Wafanyakazi wa Kiwanda cha Bia Dar es Salaam wa Mwaka 1958, April hadi Juni. Mgomo huu uliwashirikisha wafanyakazi wapatao 300, madai yao yalikuwa ni nyongeza ya mshahara. Wafanyakazi wote waliogoma walifukuzwa kazi.

Kutokana na Mgomo huu, nilishitakiwa Mahgakamani tarehe 25 April, 1958 kwa madai kwamba niliwalazimisha Makarani wawili Waafrika Kugoma. Nilitozwa faini ya Shs, 101/= ambazo Mwalimu Nyerere alilipa. Mwalimu alifanya hivyo ikiwa ni mchango wake binafsi wa kuunga Mkono Mgomo, kuimarisha uhusiano kati ya TANU na TFL, na kuwatia moyo wafanyakazi.

Ukweli ni kwamba nilikuwa mstari wa mbele katika kuongoza Migomo. Utekelezaji kwa vitendo wa falsafa ya UMOJA NI NGUVU haikuishia kwenye vyama vya wafanyakazi peke yake. Falsafa hii niliitekeleza pia katika ushirika. Baadhi yenu hamfahamu kwamba nikiwa karani wa Uhasibu, mimi pamoja na wafanyakazi wenzangu tuliokuwa tunaishi Ilala Quarters tulianzisha Chama cha Ushirika cha Walaji wa Ilala (Ilala Consumers’ Cooperative Union).

Wakati nikiwa kiongozi Serikalini na kwenye Chama nimeshiriki kwa ukamilifu katika kuhimiza na kutekeleza kwa vitendo sera ya ushirika. Chini ya TANU, ushirika uliwekewa mkazo kwa misingi kwamba ni chombo cha kuleta maendeleo. 

Ni kwa msingi huo, ndio sababu wananchi walihimizwa kuanzisha ushirika katika maeneo ambayo hayakuwa na vyama vya ushirika. Aidha, katika maeneo yaliyokuwa na vyama vya ushirika, wnanchi walihimizwa na TANU kuimarisha vyama hivyo.

Baada ya kutangazwa kwa Azimio la Arusha, ushirika umeendelea kuwa chombo cha ujenzi wa Ujamaa. Chini ya TANU na baadaye CCM, Kwakushirikiana na viongozi wenzangu nimeheimiza kwa nguvu zote uanzishaji na uimarishaji wa vyama vya ushirika, hususan vyama vya ushirika wa walaji, kuweka na kukopa, usafirishaji, maduka na ushirika wa uzalishaji mali vijijini…..,

Njia muafaka ya kuwawezesha wananchi kiuchumi ni kujiunga katika ushirika. Wananchi wasipuuze hata kidogo suala la kutekeleza sera ya Ushirika.

Usahii wa falsafa hii ya UMOJA NI NGUVU ulijidhihirisha hata wakati wa kudai uhuru wa nchi yetu. Wananchi waliungana katika mapambano dhidi ya Ukoloni wa Kiingereza. Vyama vya wafanyakazi na vyama vya Ushirika viliunga Mkono madai ya TANU ya kudai uhuru, aidha, wanachama wa vyama hivyo walihimizwa na viongozi wao kuwa wanachama wa TANU hata kwa siri kwa wale waliokuwa wanakatazwa kisheria. Kwa kutambua umuhimu wa umoja, salaam za TANU mara tu baada ya uhuru zilikuwa UHURU NA UMOJA…..

Baada ya kutangazwa kwa Azimio la Arusha, TANU ilitambua kwamba ilikuleta maendeleo ya kweli vijijini ni lazima kutumia silaha ya UMOJA NI NGUVU. Wananchi vijijini waliweza na wanaendelea kuinua hali yao ya Maisha kwa kukusanya nguvu zao.

Nilifikiri katika umri huu wa mika 78 ni vema nikawaasa viongozi wenzangu na wananchi kwa ujumla kutekeleza kwa vitendo falsafa hii ya UMOJA NI NGUVU. Binafsi naamini kwamba falsafa hii ikitekelezwa kwa ukamilifu, Taifa letu litapiga hatua kubwa zaidi kimaendeleo.

Falsafa hii, kama zilizvyo falsafa nyingine, utekelezaji wake utategemea sana uongozi. Viongozi ni lazima wawe mfano mzuri kwa wnanchi kwa maisha yao na vitendo vyao. Chama chetu cha Mapinduzi, kinatamka bayana kwamba kila kiongozi mahali alipo aoneshe nadharia ya maendeleo na vitendo kwa kuongoza kwa kutenda…

Waheshimiwa Mabibi na Mabwana ….., na fahamu kwamba mmeacha kazi zenu muhimu, hasa viongozi wa kitaifa, ilikuja kujumuika na familia ya Mzee Kawawa. Kwetu sisi huu ni upendo wa hali ya juu na niutekelezaji wa falsafa ya UMOJA NI NGUVU. Bila umoja wenu shuguli ya leo isingefanyika na kufanikiwa.

Mimi Mzee wenu nimefarijika sana kwa moyo wenu wa upendo. Sina cha kuwalipa ila kumwomba Mwenyezi Mungu awazidishie upendo.

Baada ya Kusema haya Machache, nasema tena asanteni sana kwa kushiriki pamoja nami katika sherehe ya kutimiza miaka 78 ya kuzaliwa kwangu”. Mwisho wa hotuba aliyoitoa Februari 27, 2004.

0 comments:

Post a Comment