4x4

SABODO: UKARIBU WANGU NA MWALIMU NYERERE ULIOKOA TAIFA

Sabodo
Hayati Mwalimu Nyerere
 Mwandishi Maalum
Jina la mfanyabiashara maafuru hapa Tanzania, Mustafa Jaffer Sabodo, likitajwa siyo geni masikioni mwa wengi.

Hii ni kutokana na mchango wake kwa jamii katika kuliondoa taifa kutoka sehemu moja ya chini kwenda juu, yaani maendeleo.

Sabodo mfanyabiashara maarufu ambaye ni Mtanzania mwenye asili ya Asia amekuwa akitoa mchango kwa maendeleo ya Taifa katika nyanja mbalimbali kuanzia za uchumi, siasa, elimu, afya na maji.

Mfanyabiashara huyo ambaye ni mzaliwa wa mkoani Lindi takriban miaka 73 iliyopita amejitolea kujenga shule mbalimbali nchini, hospitali, visima vya maji hata kufadhili shughuli za kisiasa na kiuchumi.

Michango yake hiyo kwa jamii ya Watanzania, imefanya jina lake kuandikwa katika mioyo ya wananchi wengi kwani alidhirisha tabia yake isiyojificha ya uzalendo kwa Taifa lake Tanzania.

Sabodo anatajwa kuwahi kuvifadhili vyama vya siasa vya CCM na Chadema kwa nyakati tofauti.

Pia anatajwa kwamba alikuwa rafiki wa karibu wa Mwalimu Julius Nyerere na wanasiasa mbalimbali nchini hata kuwahi kutumwa kwenda nchini Iran kukutana na kuomba mafuta kwa aliyekuwa kiongozi wa taifa hilo la Kiislamu, Ayatolah Khomein katika miaka ya 1970 baada ya taifa kukumbwa na uhaba wa mafuta uliochagizwa na sababu mbalimbali ikiwamo ukosefu wa fedha za kigeni.

Hali hiyo ilitokea kipindi hicho wakati dunia ilikuwa bado ikishuhudia mgawanyiko kwa baadhi ya nchi kuegemea Marekani kisiasa na kimfumo, nyingine zikifuata mfumo wa iliyokuwa Muungano wa nchi za Kisovieti za Urusi (USSR).

Si hivyo tu kwa kusoma alama za nyakati, baadhi ya nchi zilikaa kando na utengano huo na kuanzisha Jumuia ya Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote.

Miungoni mwa mataifa yaliyofuata siasa za kutofungamana na upande wowote, Tanzania wakati huo chini ya uongozi wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ilikuwa mojawapo.

Tofauti hizo za kisiasa hata kidini kati ya mataifa zilisababisha athari zilizozaa tofauti ya hali hasa kiuchumi na kisiasa hata baadhi ya nchi kuingia kwenye mahangaiko ikiwamo Tanzania iliyokumbwa na uhaba wa mafuta ya Petroli na fedha za kigeni.

Sabodo anasimulia kwamba kufuatia hali hiyo iliyoilazimu Serikali kuzuia magari yake kutembea Jumapili huku Jumamosi yakitembea hadi saa nane mchana, alipata nafasi ya kukutana na Rais Nyerere.

Anasimulia kwamba katika mazungumzo hayo alimwabia Rais Nyerere haja yake ya kutaka kwenda Iran kuomba mafuta.

“Nikamwambia wacha niende Iran. Nilifanya hivyo nikiamini Khomein atanisikiliza. Nakumbuka nilikwenda na Chifu Adam Sapi Mkwawa,” anasema.

Anasimulia: “Mimi ni Khoja, Mwislamu wa dhehebu la Shia na Khomein pia, nilipokutana naye, nikamwambia wanaoteseka Tanzania kwa shida ya mafuta wamo piaWaislamu wa Shia wengi tu.”

“Nilimwambia Tanzania ni nchi nzuri haina ubaguzi na Rais Nyerere ni mtu mwema, hata Waziri Mkuu wake ni Rashid Kawawa na Waziri wa Madini na Mafuta ni Anoor Kassam, nikamwangukia miguuni nikiliaa kuomba aipe nchi yetu mafuta, akakubali” anakumbuka Sabodo.

Hata hivyo, anasema licha ya kukubali, Khomein  akasema hawezi kumpa mafuta yeye Sabodo hadi watu wa Serikali ya Tanzania watakapofika Iran kuthibitisha ombi hilo.

“Nikarudi Tanzania na kumpa taarifa baba wa Taifa naye alimwambia Kawawa na John Malicela ikakubalika tukaenda tena Iran safari hii nikiwa na mawaziri wa Fedha, Cleopa Msuya, Anoor Kassam wa Mafuta na Usafirishaji pia alikuwepo Peter Noni kwa niaba ya Benki Kuu na Adam Sapi Mkwawa,” anasema.

Sabodo anakumbuka kuwa safari hiyo ilizaa matunda kwani Khomein aliipa Tanzania mafuta yenye thamani ya Dola za Kimarekani 80,000.

“Nakumbuka hapo urafiki wangu na Nyerere uliniwezesha kuliokoa Taifa kwa kupata mafuta baada ya kunituma kwenda Iran nilipomshauri,” anasema Sabodo ambaye wazazi wake alizaliwa Lindi.

Anakumbuka kuwa pia katika safari hiyo alimshauri Khomein kufungua ofisi ya Ubalozi wa Iran nchini naye alikubali na alifanya hiyo pia kwa Zambia, Tanzania nayo ikafungua ubalozi Iran.
Aliyekuwa Kiongozi wa Taifa la Iran, Ayatolah Khomein 

HOTUBA YA MWISHO YA UZALENDO YA HAYATI MZEE KAWAWA AKISHEREHEKEA MIAKA 78

NA HAMISI SHIMYE-UPL
“Historia ya Maisha yangu ni ndefu kama ilivyokwisha elezwa. Nilizaliwa Kijijini, nikasoma Kijijini na mjini na nikafanya kazi vijijini na mjini. Katika Maisha yangu yote nimetekeleza kwa nadharia na vitendo falsafa ya UMOJA Ni NGUVU. Vitendo vimejidhihirisha zaidi katika vyama vya wafanyakazi, vyama vya ushirika na katika vyama vya siasa, hususan Tanganyika African National Union (TANU) na Baadaye Chama cha Mapinduzi (CCM). Katika Utendaji kazi, nilizingatia falsafa hii ya UMOJA NI NGUVU”.

Nikiwa na umri wa mika 23 na mtumishi Serikalini, nilijiunga na Chama cha Watumishi Waafrika Serikalini (Tanganyika African Government Servats’ Association-TAGSA). Nilijiunga na chama hicho cha wafanyakazi kwa imani kwamba UMOJA NI NGUVU. Sikuona njia nyingine ya kupambana na dhuluma za Mkoloni kwa wafanayakazi Waafrika ila kuungana na kuanzisha vyama vya wafanyakazi.

Niliamini kwamba wafanyakazi Waafrika kwa kujiunga pamoja chini ya vyama vya wafanyakazi wangeweza kupigania maslahi na haki zao kwa nguvu kubwazaidi.

Kwa kuzingatia falsafa ya UMOJA NI NGUVU, vyama vya wafanyakazi viliunda Shirikisho la vyama vya Wafanyakazi (Tanganyika Federation of Labour- TFL), tarehe 10 Oktoba,1955. 

Mimi nilichaguliwa na wenzangu kuwa katibu Mkuu wa TFL wakati huo nikitokea Chama cha Watumishi Waafrika serikalini (TAGSA).
Nilichaguliwa kwa sababu ya ujasiri na ushupavu wangu katika kupigania haki na maslahi ya Wafanyakazi kupitia Chama cha Watumishi Waafrika Serikalini (TAGSA).

Kazi ya kwanza ya TFL ilikuwa ni kuviunganisha vyama vidogo vya wafanyakazi na kuviimarisha kwa madhumini ya kuwa na nguvu na sauti kubwa zaidi. TFL haikuwa Muuongano wa Vyma vya Wafanyakazi bali Shirikisho. Vyama hivyo chini ya shirikisho viliendelea kuendesha shughuli zake vyenyewe kama vyama vilivyokuwa na madaraka kamili juu ya wanachama wake.

Kazi ya kuviunganisha na kuvisimamia vyama vya wafanyakazi chini ya TFL haikuwa ndogo hata kidogo. Nililazimika kuacha kazi Serikalini tarehe 6 Machi, 1956 ili kutumia uwezo na muda wangu wote katika kutekeleza hiyo.

Katika Kupigania Maslahi ya wanachama wake, TFL ilitumia migomo kama silaha kubwa. Migomo mingi lifanyika lakini napenda kuzungumzia kidogo mgomo wa Wafanyakazi wa Kiwanda cha Bia Dar es Salaam wa Mwaka 1958, April hadi Juni. Mgomo huu uliwashirikisha wafanyakazi wapatao 300, madai yao yalikuwa ni nyongeza ya mshahara. Wafanyakazi wote waliogoma walifukuzwa kazi.

Kutokana na Mgomo huu, nilishitakiwa Mahgakamani tarehe 25 April, 1958 kwa madai kwamba niliwalazimisha Makarani wawili Waafrika Kugoma. Nilitozwa faini ya Shs, 101/= ambazo Mwalimu Nyerere alilipa. Mwalimu alifanya hivyo ikiwa ni mchango wake binafsi wa kuunga Mkono Mgomo, kuimarisha uhusiano kati ya TANU na TFL, na kuwatia moyo wafanyakazi.

Ukweli ni kwamba nilikuwa mstari wa mbele katika kuongoza Migomo. Utekelezaji kwa vitendo wa falsafa ya UMOJA NI NGUVU haikuishia kwenye vyama vya wafanyakazi peke yake. Falsafa hii niliitekeleza pia katika ushirika. Baadhi yenu hamfahamu kwamba nikiwa karani wa Uhasibu, mimi pamoja na wafanyakazi wenzangu tuliokuwa tunaishi Ilala Quarters tulianzisha Chama cha Ushirika cha Walaji wa Ilala (Ilala Consumers’ Cooperative Union).

Wakati nikiwa kiongozi Serikalini na kwenye Chama nimeshiriki kwa ukamilifu katika kuhimiza na kutekeleza kwa vitendo sera ya ushirika. Chini ya TANU, ushirika uliwekewa mkazo kwa misingi kwamba ni chombo cha kuleta maendeleo. 

Ni kwa msingi huo, ndio sababu wananchi walihimizwa kuanzisha ushirika katika maeneo ambayo hayakuwa na vyama vya ushirika. Aidha, katika maeneo yaliyokuwa na vyama vya ushirika, wnanchi walihimizwa na TANU kuimarisha vyama hivyo.

Baada ya kutangazwa kwa Azimio la Arusha, ushirika umeendelea kuwa chombo cha ujenzi wa Ujamaa. Chini ya TANU na baadaye CCM, Kwakushirikiana na viongozi wenzangu nimeheimiza kwa nguvu zote uanzishaji na uimarishaji wa vyama vya ushirika, hususan vyama vya ushirika wa walaji, kuweka na kukopa, usafirishaji, maduka na ushirika wa uzalishaji mali vijijini…..,

Njia muafaka ya kuwawezesha wananchi kiuchumi ni kujiunga katika ushirika. Wananchi wasipuuze hata kidogo suala la kutekeleza sera ya Ushirika.

Usahii wa falsafa hii ya UMOJA NI NGUVU ulijidhihirisha hata wakati wa kudai uhuru wa nchi yetu. Wananchi waliungana katika mapambano dhidi ya Ukoloni wa Kiingereza. Vyama vya wafanyakazi na vyama vya Ushirika viliunga Mkono madai ya TANU ya kudai uhuru, aidha, wanachama wa vyama hivyo walihimizwa na viongozi wao kuwa wanachama wa TANU hata kwa siri kwa wale waliokuwa wanakatazwa kisheria. Kwa kutambua umuhimu wa umoja, salaam za TANU mara tu baada ya uhuru zilikuwa UHURU NA UMOJA…..

Baada ya kutangazwa kwa Azimio la Arusha, TANU ilitambua kwamba ilikuleta maendeleo ya kweli vijijini ni lazima kutumia silaha ya UMOJA NI NGUVU. Wananchi vijijini waliweza na wanaendelea kuinua hali yao ya Maisha kwa kukusanya nguvu zao.

Nilifikiri katika umri huu wa mika 78 ni vema nikawaasa viongozi wenzangu na wananchi kwa ujumla kutekeleza kwa vitendo falsafa hii ya UMOJA NI NGUVU. Binafsi naamini kwamba falsafa hii ikitekelezwa kwa ukamilifu, Taifa letu litapiga hatua kubwa zaidi kimaendeleo.

Falsafa hii, kama zilizvyo falsafa nyingine, utekelezaji wake utategemea sana uongozi. Viongozi ni lazima wawe mfano mzuri kwa wnanchi kwa maisha yao na vitendo vyao. Chama chetu cha Mapinduzi, kinatamka bayana kwamba kila kiongozi mahali alipo aoneshe nadharia ya maendeleo na vitendo kwa kuongoza kwa kutenda…

Waheshimiwa Mabibi na Mabwana ….., na fahamu kwamba mmeacha kazi zenu muhimu, hasa viongozi wa kitaifa, ilikuja kujumuika na familia ya Mzee Kawawa. Kwetu sisi huu ni upendo wa hali ya juu na niutekelezaji wa falsafa ya UMOJA NI NGUVU. Bila umoja wenu shuguli ya leo isingefanyika na kufanikiwa.

Mimi Mzee wenu nimefarijika sana kwa moyo wenu wa upendo. Sina cha kuwalipa ila kumwomba Mwenyezi Mungu awazidishie upendo.

Baada ya Kusema haya Machache, nasema tena asanteni sana kwa kushiriki pamoja nami katika sherehe ya kutimiza miaka 78 ya kuzaliwa kwangu”. Mwisho wa hotuba aliyoitoa Februari 27, 2004.

RAIS DK. MAGUFULI AMTUMBUA MKURUGENZI MTENDAJI TANESCO LEO

Na Bashur Nkoromo, Dar
Rais Dk. John Magufuli, leo amemtumbua Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mhandisi Felchesmi Mramba, katika hali inayoonesha kuwa Rais amekerwa na jaribio la Tanesco kupandisha bei ya umeme kuanzia leo, Januari Mosi, 2017.

Taarifa iliyotolewa leo na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu jijini Dar es Salaam, imesema, kufuatia kutenguliwa kwa uteuzi huo, Rais Magufuli amefanya 'bandika pandua' kwa kumteua Dk. Tito Esau Mwinuka kuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO.

"Kabla ya uteuzi huo Dk. Tito Esau Mwinuka alikuwa Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM)
Uteuzi wa Dkt. Tito Essau Mwinuka unaanza mara moja", imesema taarifa hiyo ya Ikulu iliyosainiwa ana Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Gerson Msigwa.

Hatua ya Rais Magufuli, imekuja ikiwa ni siku mbili baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuiidhinisha ongezeko la asilimia 8.5 ya ya bei ya huduma za umeme kwa kilichoelezwa kuwa lengo ni kukidhi gharama za uzalishaji wa umeme.

Ongezeko hilo lilitangazwa juzi jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngamlagosi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maombi ya kurekebisha bei za umeme ambayo yalitarajiwa kuanza kutekelezwa leo, Januari Mosi, 2017.

Ngamlagosi alisema, kuwa TANESCO iliomba kuidhinishiwa ongezeko la bei ya huduma hizo ili kuliwezesha shirika hilo kupata fedha za kulipia gharama za uendeshaji, kupata fedha za uwekezaji katika miundombinu pamoja na kuhakikisha huduma ya umeme inawafikia asilimia 75 ya wananchi wote ifikapo mwaka 2025.

”Baada ya TANESCO kuwasilisha taarifa zinazohitajika kwa ajili ya kukamilisha maombi yao, EWURA ilifanya mikutano ya taftishi, matangazo kwa umma pamoja na kushirikisha wadau mbalimbali kutoa maoni juu ya ongezeko hilo ambapo baada ya uchambuzi wa maoni hayo tulilidhia kuongeza asilimia 8.5 tu ya ongezeko la bei hizo ,” alisema Ngamlagosi.

Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) ambalo linanunua umeme wa jumla kupeleka Zanzibar limeongezewa asilimia 5.7 ya bei ya umeme badala ya asilimia 19.1 iliyoombwa na TANESCO.

Alisema kulingana na marekebisho yaliyofanyika, jumla ya mapato yanayohitajika kwa mwaka 2017 ni sh. bilioni 1,608.47 ambayo yamesababisha ongezeko la bei la wastani wa asilimia 8.5 hivyo gharama za umeme zimeongezeka kutoka sh. 242.34 kwa uniti moja hadi sh.  263.02 kwa uniti moja.

Mkurugenzi huyo alitoa maagizo kwa TANESCO yakiwemo ya kuanzisha tozo ya mwezi ya sh. 5,520 kwa wateja wa kundi linalohusisha viwanda vidogo, mabango na minara ya mawasiliano, kuboresha huduma kwa wateja pamoja na kuacha kuwaunganisha wateja wadogo kwenye kundi la wateja wakubwa na badala yake kuwaunganisha moja kwa moja katika kundi la wateja wadogo.

Aliwataka wananchi kuelewa kuwa kundi linalojumuisha wateja wa majumbani ambao matumizi yao ya umeme hayazidi uniti 75 kwa mwezi hawataathirika na ongezeko hilo la bei.

Uchunguzi uliofanywa na Mtadao huu, umebaini kuwa zipo familia nyingi zenye uwezo mdogo ambazo kwa mwezi matumizi yake ya umeme hufikia hadi uniti 150 kwa mwezi, na pia tofauti na inavyoeleza kuwa wananchi wa kawaida wasigeathirika na kupanda kwa bei hiyo ya umeme, maoni ya wadau yameonyesha kuwa watu hao wangeathirika kutokana na bei za bidhaa ambazo zingepanda bei kufidia gharama ya umeme.