4x4

REA YAWEZESHA WANANCHI KUANZISHA MIRADI YA KIUCHUMI VIJIJINI

Na Jovina Bujulu-MAELEZO
USAMBAZAJI wa nishati ya umeme unaofanywa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umewezesha Wananchi wengi walioko vijijini kuanzisha miradi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa REA nchini Dkt. Lutengano Mwakahesya, nishati bora inachangia ukuaji wa uchumi wa Taifa jambo ambalo linasaidia kuboresha hali ya maisha ya Wananchi wengi walio vijijini. Kwa kutambua umuhimu huo REA kwa kushirikiana na Wadau mbalimbali imeweza kuibua miradi mbalimbali ya nishati vijijini ili Wananchi waweze kufaidika nayo.

Wadau hao ni pamoja na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO), Mamlaka ya Udhibiti wa Bei za Bidhaa (EWURA), Wizara ya Nishati na Madini, Asasi zisizo za Kiserikali (AZISE), Asasi za Kijamii (AZAKI) na Sekta binafsi. Dkt. Mwakahesya ameainisha miradi ya nishati za umeme kuwa ni pamoja na zile zinazotumia nguvu ya upepo, jua, maji na bayogasi.

Dkt. Lutengano ameeleza kwamba, lengo kubwa la ushirikiano baina ya REA na Wadau hao ni kuibua miradi mbalimbali ya nishati,  kutoa ruzuku na kuwezesha upatikanaji wa ushauri wa kitaaluma kwa waendelezaji wenye sifa katika masuala ya kiufundi, usimamiaji, uchanganuzi wa kifedha,  ugharamiaji wa miradi na mienendo mizuri ya miradi hiyo.  

Amesema, REA inahakikisha kwamba uendelezaji wa miradi ya nishati vijijini unazingatia utumiaji wa mazingira ili kutunza vyanzo vingine vya nishati. Ameongeza kusema kuwa REA inaongozwa na Bodi ya Nishati vijijini ambayo husimamia uendeshaji wa Mfuko wa Nishati vijijini (REF). Mfuko huu unasaidia kuongeza kasi ya upatikanaji wa miradi ya Nishati.

Serikali kupitia mfuko wa Nishati vijijini ilifadhili miradi kabambe ya usambazaji wa umeme vijijini awamu ya kwanza na ya pili ambayo inatekelezwa na Wakandarasi binafsi katika mikoa yote ya Tanzania Bara.

Utekelezaji wa mradi huu umekamilika kwa asilimia 90 na ambapo kilometa 1600 za msongo wa kati na kilometa 97 za msongo mdogo zimejengwa na vipoza umeme vilifungwa na wateja wa awali 18,253 wameunganishiwa umeme.

Katika awamu ya pili mradi ulilenga kujenga vituo 6 vya kuongeza msongo wa (umeme 11/33 KV) katika miji ya Kigoma, Kasulu, Kibondo, Ngara, Mbinga na Tunduru, ujenzi wa njia za umeme msongo mdogo na wa kati na kufunga mashine umba (transfomer) 3100. Mradi ulilenga kuunganisha wateja 225,000 na vijiji 2,500 pindi ukikamlika na kupeleka  umeme makao makuu ya Wilaya 13.

Mradi huu uliweza kujenga vituo 6 vya kuongeza nguvu Kigoma Vijijini, Kasulu, Kibondo, Ngara, Mbinga na Tunduru.Aidha mradi ulikamilisha ujenzi wa njia za msongo mdogo na wa kati,na wateja 61,023 walipatiwa umeme. Jumla ya vijiji 1,162 viliunganishwa kwenye gridi. 

Akielezea juu ya shughuli za kiuchumi na kijamii zilizoanzishwa vijijini Dkt. Lutengano amesema, kutokana na upatikanaji  wa nishati ya umeme vijijini maisha ya Wananchi yamekuwa mazuri kutokana na kuwepo kwa shughuli za kibiashara kama vile, mashine za kusaga na kukoboa nafaka, viwanda vya uselemala, utengenezaji wa milango na madirisha ya chuma, uuzaji wa vinywaji baridi n.k.

Kwa upaande wa shuhguli za kijamii, upatikanaji wa nishati wa umeme umeboresha huduma za hospitali, vituo vya afya na kumeongezeka kwa ari ya wanafunzi kujisomea wakati wote na pia matumizi ya kompyuta mashuleni, Kwa sasa wanawake wajawazito wanakwenda hoapitalini kujifungua bila kulazimika kuchukua  koroboi. 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara ya Nishati na Madini, hadi mwaka 2014 kiwango cha uunganishaji umeme katika Makao Makuu ya Wilaya na vijijini ulifikia asilimia 24 na kufanya Wananchi wanaopata huduma za umeme kufikia asilimia 36 ya Watanzania  waishio  bara ukilinganisha na mwaka 2005 ambapo kiwango cha uunganishaji umeme kilikuwa chini ya asilimia 10.

Raarifa hiyo inaonesha kwamba ongezeko hilo linatokana na juhudi mbalimbali za Serikali ikiwa ni pamoja na kuanzishwa kwa Wakala wa Nishati vijijini (REA) na kupunguza gharama za kuunganisha umeme wa njia moja na kuhamasisha Wananchi kutumia umeme. 

Jumla ya shule za sekondari 1845, zahanati na vituo vya afya 898  na hospitali 96 zimepatiwa huduma ya umeme katika maeneo mbalimbali nchini. Aidha, Wakala kwa kushirikiana na TAZAMA pipeline na Mfuko wa Maendeleo wa Mafia umewezesha utekelezaji wa miradi miwili ya kupeleka umeme katika pampu za kusukuma maji na mafuta za TAZAMA zilizoko Kisanga (Morogoro).

Akizungumzia mafunzo yanayofadhiliwa na Wakala kwa wananchi, Meneja wa Tathmini na Ufuatiliaji wa REA , ndugu Vestina Rwelengera alisema kwamba ni pamoja na kuwapatia mafunzo yote ya nishati, mfano utunzaji wa vyakula  kwa kutumia nishati ya jua, miradi ya umwagiliaji, kukausha samaki na mboga mboga.

Alitaja maeneo yaliyonufaika na  na mafunzo hayo kuwa ni Bagamoyo, Mafia na Somanga Fungu ambapo wananchi walipata mafunzo ya kutengeneza mkaa kwa kutumia majani makavu. Pia  Wakala kupitia mfuko wa Nishati Vijijini, ulitoa ruzuku kwa vikundi vinavyotayarisha maandiko ya miradi ili kuwawezesha wanavijiji kupata mikopo kutoka kwenye benki zilizokubaliana na Mfuko huo. 

Akizungumzia miradi mingine iliyotekelezwa na inayoendelea kutekelezwa ya usambazaji wa umeme vijijini ndugu Vestina aliema kwamba ni pamoja na mradi wa SAGCOT Cluster ambao utasambaza umeme kilometa 100 , kujenga kituo cha  kupozea umeme katika mji wa Ifakara na mradi huu utaunganisha wateja 3,000.

Miradi mingine ni ya Andoya ( Mbinga), Tulila (Songea), Yovi (Kilosa), ambayo imeanza uzalishaji. Miradi ya Maguta ( Kilolo), Lupali (Njombe), na Isigula (Ludewa) ambayo imeanza kazi ya ujenzi na miradi ya Mwenga (Mufindi) ambapo jumla ya wateja zaidi ya 4,600 wameunganishwa.

Hadi kufikia Desemba 2015  vijiji 5,009 ambavyo ni sawa na asilimia 33 vilikuwa vimeunganishwa na huduma za umeme  na miradi inayoendelea itaunganisha vijiji vingine vipya 1,340 na kufanya jumla  ya vijiji 6,349 kupata huduma ya umeme miradi ikikamilika.

Akizungumzia changamoto zinazoikabili Wakala, ndugu Vestina alisema kuwa ni pamoja na Wananchi wa vijijini kushindwa kumudu gharama za kuunganishiwa umeme, upatikanaji wa rasilimali fedha za kutosha na usalama wa miundombinu kutokana na uharibifu na vitendo vya uharibifu vinavyofanywa na wananchi.

0 comments:

Post a Comment